Jumanne, 20 Februari 2018

TAJIRI MOSHI AKAMATWA NA MAPIPA KUMI YA KEMILAKI ZA HATARI,NI WIFRED LUCAS TARIMO


JESHI  la polisi mkoani Kilimanjaro,limemtia mbaroni mfanyabiashara  maarufu katika miji ya Moshi na Arusha,Wilfred  Lucas Tarimo  kwa kutuhuma za kukutwa na mapipa kumi yaliyosheheni kemikali bashirifu zilizopigwa marufuku na serikali.

Tarimo ambaye pia ni mmoja wa wakurugenzi wa Kampuni ya Derrick Global Trading(D.G.T) ya mjini Moshi  watengenezaji wa pombe aina ya banana kupitia kinywaji chake cha Budget,alikamatwa hivi karibuni na polisi pamoja na mkewe aliyetajwa kwa jina moja la Irene.

Kaimu kamanda wa polisi mkoani Kilimanjaro,Koka Moita alidhibitisha kukamatwa kwa mfanyabaishara huyo alipozungumza na mtandao huu na kwamba upelelezi juu ya tuhuma hizo unaendelea.

Kwa mujibu wa kamanda Koka,tayari ofisi ya Mkuu wa upelelezi wa makosa ya jinai mkoa(RCO) imemwandikia barua mkemia mkuu wa serikali kwa ajili ya kufanyia uchunguzi wa kimaabara kemmikali hizo na kubaini aina ya kemikali husika pamoja na thamani yake.

“Ni kweli hilo tukio la Wilfred Tarimo lipo,amekamatwa na mapipa kumi ya kemikali na nimezungumza na  RCO amesema tayari wameshamwandikia barua mkemia mkuu wa serikali li waje kuzifanyia uchunguzi wa kimaabara hizo kemikali na hapo ndipo tutajua aina ya kemikali na thamani yake kabla ya hatua zaidi za kisheria kuchukuliwa”,alisema Koka.

Mtandao huu  umezungumza na mkemia mwandamizi wa serikali kanda ya Kaskazini,Christphera Anyango kutaka kujua namna wanavyopokea sampuri kwa ajili ya uchunguzi wa kimaabara.

Kwa mujibu wa Anyango,ofisi yao hupokea sampuli mbali mbali kutoka polisi na kuzifanyia uchunguzi na kwamba pia wanaweza kuchukua sampuli wenyewe kulingana na mahitaji ya wahusika.

“Polisi wanaweza wakaleta sampuli wenyewe na kama kuna kitu kinahitaji utaalamu zaidi wanatuandikia barua na sisi tunakwenda kuchukua wenyewe na kuzifanyia uchunguzi”,alisema.

Alipoulizwa kama wameshapokea barua kutoka ofisi ya mkuu wa upelelezi wa makosa ya jinai(RCO) mkoa wa Kilimanjaro kwa ajili ya kwenda kuchukua sampuli za kemikali zilizokamatwa kwa mfanyabiashara huyo,ofisa huyo alisema yupo nje ya ofisi.

Hata hivyo aliomba atafutwe ofisa mwenzake  aliyemwachia ofisi aliyetajwa kwa jina la Joyce Njisya ambaye amekiri kupokea barua hiyo kutoka polisi Kilimanjaro alipozungumza na Jamhuri.

Akizungumza na mtanao huu  kwa nija ya simu,Joyce amesema kuwa yatari wameshachukua sampuli za kemikali hizo na kuzituma makao makuu ya ofisi ya mkemia mkuu wa serikali kwa ajili ya uchunguzi wa kimaabara.

“Ni kweli hiyo barua tumeshaipokea na tumeshachukua sampuli na kuzipeleka makao makuu yetu kwa ajili  ya uchunguzi,tukikamilisha uchunguzi wetu tutarejesha majibu ya uchunguzi kwa polisi,wao ndo watakuwa kwenye nafasi nzuri ya kuyatolea majibu”,alisema.


Hata hivyo mfanyabiashara huyo hakukiri wala kukanusha kukamatwa na shehena ya kemikali zilizopigwa  marufuku na serikali kwani baada ya kupigiwa simu alidai yupo kwenye kikao na aliahidi kuwasiliana na mwandishi wa habari hizi mara baada ya kikao hicho lakini hakufanya hivyo.

Na hata alipotumiwa ujumbe mfupi wa maandishi kupitia simu yake ya kiganjani,bado mfanyabiashara huyo hakuweza kujibu maswali aliyoulizwa na mwandishi wa habari hizi.

“Mr.Wilfred Tarimo habari za leo?,naitwa Charles Ndagulla mwandishi wa habari gazeti la Jamhuri,unazungumziaje tuhuma za wewe na mke wako Irene kukamatwa na polisi mkituhumiwa kukutwa na mapipa kumi yenye kemikali bashirifu zilizopigwa marufuku na serikali?,unasomeka ujumbe huo.

Kukamatwa kwa mfanyabiashara huyo kunakuja siku chache baada ya maofisa wa Mamlaka ya  Chakula la Dawa(TFDA)Kanda ya kaskazini,kukifunga kiwanda hicho cha kutengeneza pombe aina ya Banana cha Derrick Global Trading(D.G.T ) baada ya  kubainika kuwa na kasoro .

Kiwanda hicho kilifungwa chini ya kifungu cha 181 sura ya 209 ya sheria ya chakula na dawa ya mwaka 2003 kutokana na tuhuma za kutumia nembo ya kiwanda kingine cha kutengeneza pombe kali kinyume cha sheria.

Akizungumza na waandishi wa habari kiwandani hapo hivi karibuni,Mkaguzi wa chakula mwandamizi kutoka TFDA Kanda ya kaskazini,William Mhina,alisema sababu nyingine za  kufungwa kwa kiwanda hicho ni mazingira yasiyoridhisha ya kiwanda hicho.

Alitaja sababu zingine ni wafanyakazi kutokuwa na vyeti vya kuonyesha afya zao huku wafanyakazi hasa wa kike kutokuvaa kofia kichwani.

Alisema uchunguzi wao umebaini kuwa,eneo la kuoshea chupa ni chafu na kwamba chupa hizo zimekuwa zikioshwa katika mazingira yasiyoridhisha.

Alisema wamiliki wa kiwanda hicho wamepewa muda wa kurekebisha kasoro hizo na baada ya kufanya hivyo TFDA itafanya ukaguzi tena kujiridhisha kama kasoro hizo zimefanyiwa kazi,

Mbali na kufungwa kwa kiwanda hicho,jeshi la polisi kwa kushirikiana na maofisa wa mamlaka ya mapato Tanzania(TRA),walifanikiwa kukamata shehena ya vifungashio  vinavyotumiwa na kampuni moja mkoani Shinyanga  ya Canon General Supply inayojihusisha na utengenezaji wa pombe kali aina ya Shujaa.

Vifungashio hivyo vilikamatwa ndani ya kiwanda hicho kilichopo eneo la Kwa Alphone kata ya Kibolironi  huku baadhi ya wafanyakazi wa kiwanda hicho wakishikiliwa na jeshi la polisi kwa mahojiano zaidi.

Akizungumzia tukio hilo,ofisa huyo kutoka TFDA alisema hilo ni kosa kwa mujibu wa sheria inayosimamia usajili wa bidhaa na kuongeza kuwa,vifungashio vilivyokamatwa ndani ya kiwanda hicho havimo kwenye orodha ya usajili wa bidhaa zinazozalishwa na kampuni hiyo.

Kwa upande wake kamanda wa polisi mkoa wa Kilimanjaro,Hamisi Issah alisema jeshi hilo linamshikilia meneja wa Kiwanda hicho aliyemtaja kwa jina la Boniface Damas(56) pamoja na wafanyakazi watatu wa kiwanda hicho.

Kamanda Issah aliwataja wafanyakazi hao kuwani Severine Pantaleo(37),Riziki Fabian (28) na Daniel Japhet(18) ambao wanadaiwa kukutwa na pombve kali iliyofungashwa kwenye viroba iana ya Zed inayodaiwa kutengenezwa kienyeji.

“Viroba hivyo vina alama zake,lakini watuhumiwa hawa walikuwa wakitengeneza katika mfumo wanaoujua wenyewe,utengenezaji wa pombe usiozingatia taratibu ni hatari na unaweza kuleta madhara makubwa kwa wanywaji”,alisema kama Issah.

Kuhusu vifungashio vilivyokamatwa ndani ya kiwanda cha D.G.T,kamanda Issah alisema kuwa,wamiliki wa kiwanda hicho hawakuwa na haki stahiki ya kutengeneza pombe hizo kutokana na kutengeneza pombe hizo pasipo kuzungitia tararibu za kisheria.

Kamanda Issah amesema polisi kwa kushirikiana na TFDA wanafanya uchunguzi juu ya tuhuma hizo ikiwamo matumizi ya malighafi isiyo ya kiwanda hicho na uchunguzi ukikamilika sheria itachukua mkondo wake kwa watakaobainika kutenda makosa.

Hata hivyo tangu kukamatwa kwa watuhumiwa hao  uchunguzi wa Jamhuri umebaini kuwa mpaka sasa hawafikishwa mahakamani.





MWISHO

Alhamisi, 15 Februari 2018

MTUMISHI MKOMBOZI BANKI AIBA MAMILIONI YA WATEJA,NAYE ALIZWA NA MATAPELI


 Na Charles Ndagulla,Moshi.

MTUMISHI mmoja wa benki ya kibiashara ya Mkombozi tawi la Moshi(jina tunalihifadhi),anatuhumiwa kuiba zaidi ya shilingi Milioni 57 kutoka kwenye akaunti za wateja wa benki hiyo.

Habari za uhakika ambazo mtandao huu umezipata zimedai kuwa,mtumishi huyo aliiba fedha hizo kati ya Oktoba na Desemba mwaka jana lakini polisi wameshikwa kigugumizi kuanika majina ya wateja waliolizwa fedha zao.

Taarifa kutoka ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali mjini Moshi,zinapasha kuwa,polisi wamekataa kuweka wazi majina ya wateja hao,akaunti zao na kiasi cha fedha kilichoibwa na mtumishi huyo.

Inadaiwa kuwa,kugoma kwa polisi kuweka majina ya wateja hao,kumeikwamisha ofisis hiyo ya mwanasheria mkuu wa serikali kuandaa hati ya mashitaka ili mtumishi huyo aweze kufikishwa makahamani.

Hata hivyo taarifa zinapasha kuwa,mtumishi huyo hakuweza kunufaika na mamilioni hayo ya wateja baada ya kuingizwa 'mjini' na matapeli waliomhadaa kuwa fedha hizo zitaongezeka mara dufu.

Kwa lugha nyepesi mtumishi huyo aliponzwa na uroho wa kupata utajiri wa chap chap bila kuutolea jasho na sasa yupo kikaangoni kwani anakabiliwa na tishio la kufukuzwa kazi wakati wowote.

Kwa taarifa zaidi juu ya sakata hilo enedelea kutembelea mtandao huu.

Jumatatu, 5 Februari 2018

TAPELI ANAYEISHI KWA KUTUMIA MAJINA YA VIONGOZI MBARONI


Jeshi la Polisi mkoani Kilimanjaro, limemtia mbaroni mkazi wa wilaya ya Mwanga, aliyekuwa akisakwa kwa udi na uvumba kwa kutumia majina ya viongozi kutapeli fedha kwa njia ya mtandao.
Kamanda wa Polisi mkoa Kilimanjaro, Koka Moita, alisema jana kuwa mtuhumiwa huyo anashikiliwa kwa kutumia jina la aliyekuwa mkuu wa mkoa Kilimanjaro, Said Mecki Sadick kutapeli fedha.
Kaimu kamanda huyo alisema ingawa mtuhumiwa huyo alikamatwa Januari 28 kwa tuhuma za kuiba shehena ya viazi huko Tarakea wilayani Rombo, lakini alikuwa akitafutwa kwa tuhuma za utapeli.
“Anatuhumiwa kuiba viazi funzo nzima huko Tarakea Rombo lakini tulikuwa tunamtafuta kwa impersonation (kujifanya) yeye ni Said Mecki Sadick aliyekuwa mkuu wa mkoa wakati siye,”alisema.
Moita alisema mtuhumiwa huyo, Hassan Omary Kashingo, anashikiliwa kituo kikuu cha polisi Moshi na kuwataka wananchi ambao walifungua taarifa juu yake, wafike ofisi ya RCO Kilimanjaro.
Desemba 15,2015, aliwahi kukamatwa na Polisi kwa tuhuma za kutumia jina la aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi , sasa ni mwenyekiti wa bodi ya chuo cha Diplomasia, Balozi Ombeni Sefue kutapeli.
Wakati akikamatwa, tayari kulikuwa na majalada zaidi ya nane ya utapeli katika kituo cha kati mjini Moshi, na haijulikani ilikuwaje hakurejeshwa Moshi kujibu tuhuma zinazomkabili.
Kumbukumbu za Polisi, zinaonyesha kuwa mtuhumiwa huyo anatumia majina tofauti tofauti ya Hassan Abdalah au “Golota”, Yusuph Mjema au “Kashingo”, na majina mengi ambayo hayajabainika.
Novemba mwaka jana mtuhumiwa huyo anadaiwa kutumia jina Sadick kutapeli fedha kutoka kwa viongozi mbalimbali wa umma, dini na wananchi wa kawaida, akijitambulisha kuwa ni Sadick.
Aliyekuwa Kamanda wa Polisi mkoa Kilimanjaro, Wilbroad Mutafungwa alitangaza Jeshi hilo kumsaka kwa udi na uvumba mtuhumiwa huyo kwa tuhuma mbalimbali za utapeli akisajili laini ya Sadick.
Kwa upande wake, mkuu wa mkoa Kilimanjaro, Said Mecki Sadick  alilithibitishia gazeti hili mwaka jana, kupokea taarifa za kuwepo kwa mtu anayetumia jina lake kutapeli na kwamba tayari ameripoti polisi.
Mtuhumiwa huyo ndiye ambaye Desemba 4, 2015, alimpigia mhadhiri mmoja wa chuo kikuu cha St. John cha mjini, na kujifanya yeye ni Balozi Sefue, na kwamba ana shida.
Katika maongezo hayo, mtuhumiwa huyo ambaye ni mhitimu wa darasa la saba, alimuomba Profesa huyo  amtumie mtoto wake Sh500,000 ambaye amepata dharura akiwa mkoani Singida.
Hata hivyo ilibainika baadae kuwa mtu huyo hakuwa Balozi Ombeni Sefue na ndipo DCI alipounda kikosi kazi kilichopiga kambi mkoani Kilimanjaro na kufanikiwa kumtia mbaroni mtuhumia huyo.
Mtuhumiwa huyo ndiye anayetuhumiwa  kati ya mwaka 2013 na 2015, alitapeli viongozi mbalimbali kwa kutumia jina la mwandishi mwandamizi wa habari wa mkoa wa Kilimanjaro, Daniel Mjema.
 Chanzo:Mwananchi

Ijumaa, 2 Februari 2018

NABII TITO AMWIMBUA ASKOFU SHOO, AKUMBUSHIA YA KIBWETERE


Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dk. Fredrick Shoo, ameonya kuwa watu wakichanganyikiwa kwa mambo ya kiroho, madhara yake ni makubwa.

Askofu Shoo ametolea mfano wa mwaka 2000 ambapo Askofu Joseph Kibwetere wa Uganda, aliwaangamiza wafuasi wake 1,000 kwa moto baada ya kuwaaminisha kuwa mwisho wa dunia umefika.

Mkuu huyo wa kanisa ametoa kauli hiyo kufuatia kile alichosema kuongeza kwa mafundisho potofu ya dini ya kikristo, na kuipongeza Serikali kwa kumdhibiti aliyejiita Nabii Tito mkoani Dodoma.

Dk Shoo ambaye pia ni Askofu wa Dayosisi ya Kaskazini ya Kanisa hilo, alitaka taratibu za usajili wa makanisa na taasisi za dini utizamwe upya, ili kuepusha jamii kupokea mafundisho potofu.
 “Ndio maana kwa muda mrefu tumesisitiza (Serikali) watafute maoni ya mabaraza ya makanisa kabla ya kuruhusu kila mtu anayejisikia kuanzisha kanisa lake anafanya hivyo,”alisema na kuongeza;-

“Watu wakichanganyikiwa kwa mambo ya kiroho madhara yake sio kwa kanisa tu bali ni kwa jamii nzima inayopokea mafundisho hayo potofu. Chukua mfano wa Kibwetere wa Uganda”.

Kauli ya Askofu Shoo imekuja wakati polisi mkoani Dodoma wakiendelea kumshikilia Tito Machibya maarufu kwa jina la Nabii Tito, kwa madai ya kujenga chuki dhidi ya dini za watu wengine.

Kabla ya kukamatwa kwake “Nabii Tito”, alionekana katika mitandao ya kijamii, akitoa mafundisho ya dini ya kikristo, ambayo baadhi ya watu na Serikali wameyatafsiri kuwa amfundisho potofu ya kidini.

Polisi kupitia kwa kamanda wa Polisi mkoa wa Dodoma, Gilles Muroro wanadai daktari wa hospitali ya Mirembe mkoani humo, wamethibitisha kuwa “Nabii Tito” ana matatizo ya kiakili.

Lakini wakati polisi wakishughulika na Nabii Tito, kumeibuka wimbo kubwa la uanzishaji wa makanisa, ambapo baadhi ya wanayoyaanzisha hujivika vyeo vya Utume au Unabii wao na wenza wao.

Mbali na kujikita katika mafundisho ya ajabu ajabu, baadhi ya makanisa hayo yanadaiwa kujiendesha kibiashara badala ya kuhibiri Injili, huku mengine yakienda mbali na kupanga viwango vya sadaka.

Hivi karibuni, Naibu Askofu wa kanisa katoliki Jimbo la Moshi, Padre Deogratius Matiika aliliambia gazeti hili  kuwa, ujio wa makanisa mapya na wanaojiita Mitume, umekuja na changamoto na kero.
 “Baadhi wanaishi maisha ya anasa na wana utajiri mkubwa wakati miongoni mwa washirika wao kuna watu hawajui hata watakula nini baada ya kutoka ibadani na hawafahamu watasaidiwa vipi,”alisema.

Padre Matiika alisema kuwa yapo baadhi ya makanisa mengi yanatumia nguvu za giza kuwatapeli waumini wao kuwa wanaponya na kufufua watu waliokufa,hali ambayo inawagharimu waumini.

“Unakuta muumini anaambiwa alete picha ya marehemu iombewe ili afufuke na anapoileta ni lazima iambatanishwe na fedha. Huo ni utapeli mkubwa na haukubaliki,”alisema Matiika.

“Kumtolea Mungu sadaka hupangiwi unatoa kile ambacho mfukoni mwako unaoana ni chenye kumpendeza Mungu na sio kupangiwa kutoa sadaka,”alisisitiza Padre Matiika.

Padre Matiika aliiomba Serikali kuweka mwongozo na mikakati maalumu kwa makanisa ili kuepukana na kuongezeka kwa makanisa mengi ya uongo ambayo yanapotosha waumini wa leo.


Chanzo:Mwananchi