Alhamisi, 1 Februari 2018

TAKUKURU YAWAFUNGIA KAZI WATUMISHI WANAOFISADI MALI ZA UMMA


 Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), imewaburuza kortini watumishi wawili wa Halmashauri ya wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro kwa tuhuma za ufisadi.

Waliofikishwa mbele ya Hakimu Mkazi wa Moshi, Pamela Mazengo ni Nicodemus Nyaki ambaye ni karani idara ya fedha na Dk Lucas Kawishe aliyekuwa Kaimu Mganga mkuu wa Halmashauri hiyo.

Washitakiwa hao walifikishwa kortini hivi karibuni na kusomewa mashitaka manne yanayohusu kughushi nyaraka zinazohusu malipo ya Sh4.6 milioni, na mwendesha mashitaka wa Takukuru Susan Kimaro.

Mwendesha mashitaka huyo wa Takukuru alidai Novemba 4,2012, katika ofisi za kiwanda cha sukari cha TPC, washitakiwa waligushi barua wakitaka waidhinishiwe kiasi hicho cha fedha.

Fedha hizo walidai ni kwa ajili ya kuwalipa madaktari bingwa na dereva ambao walishiriki katika kliniki maalumu katika hospitali ya TPC, huku wakifahamu kuwa taarifa hizo zilikuwa ni uongo.

Katika shitaka lingine, ilidaiwa kuwa kati ya Desemba 8 na 17,2012 katika eneo hilo hilo, washitakiwa walighushi hati ya malipo namba PV001579 kuonyesha kiasi hicho cha fedha kingelipwa madaktari hao.

Halikadhalika ilidaiwa kuwa Desemba 14 mwaka huo huo, washitakiwa waligushi orodha yenye majina ambayo ilionyesha wamelipwa jumla ya Sh4.6 milioni, wakati wakifahamu orodha hiyo ni ya uongo.

Mbali na kosa hilo, lakini wanadaiwa kuwa kati ya Desemba 8 hadi 17,2012, wakiwa watumishi wa Halmashauri ya Moshi, walitumia vocha namba PV001579 ambayo ilikuwa na maelezo ya uongo.

Maelezo katika vocha hiyo yaliyoonyesha Sh4.6 milioni zililipwa kwa madaktari bingwa na dereva ambao walihudhuria klini maalum, yanadaiwa kuwa ya uongo kwa lengo la kumpotosha mwajiri.

Washitakiwa walikana mashitaka hayo na kuachiwa kwa dhamana hadi Februari 22, wakati kesi yao itakapotajwa kwa kuwa upelelezi wa makosa yao ulikuwa bado haujakamilika.


Chanzo. Mwananchi

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni