Jumatatu, 12 Januari 2015

MANISPAA YA MOSHI MATATANI, UVAMIZI NA UPORAJI USIKU WA MANANE



Halmashauri ya Manispaa ya Moshi, mkoani Kilimanjaro imeingia katika kashfa ya uvamizi na uporaji wa mali za wafanyabiashara wa Mananasi baada ya kuvamia usiku wa manane katika eneo la maegesho ya magari wakidai ushuru wa mazao hayo. 
Tukio hilo la kusikitisha lilitokea usiku wa kuamkia Desemba 19 mwaka jana katika eneo la maegesho ya magari la Manyema lililopo katika Manispaa ya Moshi.

Magari yaliyokuwa na mananasi yenye thamani ya shilingi milioni 54  yenye namba  za usajili T 884 ALF Suzuki Forward, T 667 AAM Fuso Mitsubishi na  T 149 ADD Fuso hayajulikani yalipo mpaka sasa.

Akizungumza katika eneo la tukio Mlinzi wa Kampuni la Chui Security Co. Ltd aliyefahamika kwa jina la Benjamin Mayalla alisema watu 20 wakiwemo askari wawili waliokuwa na silaha za moto walimweka chini ya ulinzi na kutakiwa kutofanya chochote mpaka wamalize kilichowaleta.

Mlinzi huyo alitii amri ya watu hao, ambao kati yao aliwabaini kuwa ni askari wa Manispaa ya Moshi waliovalia kiraia huku wakiwa na magari mawili, moja kati ya hayo lilikuwa ni ‘breakdown’

‘Majira ya saa 8 za usiku nikiwa kwenye lindo la kazi, walifika watu 20, wawili wakiwa na silaha za moto walivunja geti kwa kutumia bomba la chuma na kuingia katika eneo la maegesho na kunitaka nisalimu amri, kitu ambacho nilitii kibaya zaidi ilikuwa ni kuyafungua magari matatu kwa funguo za bandia walizokuwa nazo,’ alisema Mayalla

Mayalla aliongeza kusema magari mawili kati ya hayo yalikubali kuwaka na moja walilivuta na ‘breakdown’ hata kukwangua sehemu ya maegesho na kuyapeleka kusikojulikana.
Kwa upande wao wamiliki, madereva wa magari hayo waliojitambulisha kwa majina Absamadu Ivere, Shaban Juma na Malaki Mlay walisema walifika jioni ya Desemba 18 mwaka jana mjini Moshi wakitokea Bagamoyo kununua mananasi hayo kwa ajili ya kuyauza Jijini Arusha na Babati waliyapeleka katika eneo la maegesho kwa ajili ya kuendelea na safari siku inayofuata.

‘Alfajiri tulipofika kwa ajili ya kuendelea na safari yetu, huku tukiwa na funguo za magari tulitaarifiwa na mlinzi kuwa maaskari wa manispaa wamevamia na kuyachukua magari yote na yeye (mlinzi) kumweka chini ya ulinzi licha ya kutomdhuru wamechukua magari yetu na mzigo wetu wote (mananasi) na hatujui walikopeleka,’ alisema Absamadu  Ivere.

Pamoja na  juhudi za wafanyabiashara hao kudai kupeleka taarifa kwa mkuu wa kituo cha Polisi Moshi, Afande Kasindo aliwajibu kuwa kama waliohusika ni Askari wa Manispaa, hawana budi kutoa taarifa kwa Mkurugenzi ambako maswali mengi yakishindwa kupatiwa ufumbuzi huku Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoani Kilimanjaro Geoffrey Kamwela  akidai kutopata taarifa yoyote tangu siku ya tukio na kuahidi kulifanyia uchunguzi.

Akizungumza kwa njia ya simu Mkurugenzi wa  Halmashauri ya Manispaa ya Moshi Shaban Ntarambe amekiri kuwepo kwa tukio hilo ingawa tayari kesi hiyo imepelekwa Mahakamani.

Hata hivyo, majibu ya mkurugenzi huyo kuwa kesi hiyo imefikishwa mahakamani, yanazua utata zaidi huku wafanya biashara hao wakiwa njiapanda kwani hawajaitwa mahakama yoyote ile kutoa utetezi wao.

Itakumbukwa kwamba askari wa Manispaa ya Moshi wamekuwa na tabia ya kuchukua mali za wafanyabiashara na kisha kugawana wao kwa wao kutokana na ukweli kwamba hakuna anayefuatilia hatma ya mali zikiwa mikononi mwa mamlaka hiyo.

CHANZO: JAIZMELALEO

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni