Jumatatu, 7 Mei 2018

BASTOLA ILIYOPORWA MOSHI YATUMIKA KUUA MLINZI SHAMBA LA MKONGE KOROGWE


 JESHI  la polisi mkoani  Tanga limefanikiwa kuwatia mbaroni watu wanne akiwamo mwanamke mmoja mkazi wa Kigogo Jijini Dar es salaam wakituhumiwa kuhusika ma mauaji ya mlinzi wa shamba la Mkonge la Kwa Mduru lililopo wilaya ya Korogwe .

Katika tukio hilo,mlinzi wa shamba hilo,Omar Athuman aliuawa kwa kupigwa risasi huku meneja mkuu wa Shamba hilo ambaye ni raia wa Kigeni,Mathias Hendrik akijeruhiwa vibaya sehemu mbali mbali za mwili wake.

Kamanda wa polisi mkoa wa Tanga,Kamishna Msaidizi  Mwandamizi wa polisi(SACP),Edward Bukombe,amezungumza na Ndagullablog na kueleza  kuwa katika tukio hilo,majambazi hao mbali na kuua,kujeruhi,pia walipora vitu mbali mbali zikiwamo,pesa,simu .

Waliokamatwa kuhusiana na tukio hjilo ni Ebeni Venance Mwaipopo(27)mkazi wa Ngarenairobi mkoani Arusha,Fredrick Menadi(46) mkazi wa Chekereni ya Bonite mjini Moshi,Diana Godliving(24)na Dismas Venance Mwaipopo,wote wakazi wa Dar es salaam.

“Katika tukio hilo,watuhumiwa hao walitumia silaha ya moto kufanikisha uporaji huo ambako walimuua mlinzi wa shamba hilo,wakamjeruhi mwenzake lakini meneja mkuu wa shamba hilo naye alijeruhiwa vibaya”,amesema kamanda Bukombe.

Habari kutoka wilayani Korogwe zinadai kuwa,kutokana na meneja huyo kupata majereha makubwa sehemu mbali mbali za mwili ,kwa sasa yuko nchini Afrika Kusini kwa ajili ya matibabu zaidi.

Akizungumza na Ndagullablog ofisini  kwake hivi karibuni,kamanda Bukombe alisema uchunguzi wa polisi umebaini kuwa silaha iliyotumika katika tukio hilo la mauaji ya mlinzi huyo iliibwa mkoani Kilimanjaro.

Kwa mujibu wa kamanda Bukombe,Bastola hiyo aina ya Norinco Star,ni mali ya mfanyabiashara Denis Swai mkazi wa Soweto katika Manispaa ya Moshi  mkoani Kilimanjaro.

Ndagullablog imezungumza na Swai ambaye amekiri kuwa Bastola hiyo ni mali yake na kwamba tayari ameshaitwa na ofisi ni Mkuu wa upelelezi wa makosa ya jinai(RCO) mkoa wa Tanga kwa ajili ya utambuzi.

“Kama ulivyopata taarifa kwa RPC wa Tanga ni kweli hiyo bastola ni mali yangu na hivi karibuni niliitwa na RCO kwenda kuitambua na nimejiridhisha kuwa ni mali yangu japo imefutwa namba”,amesema Swai.

Mfanyabiashara huyo amesema kuwa,bastola hiyo iliibwa na watu wanaaminika kuwa ni majambazi baada ya kuvamia nyumbani kwake eneo la Soweto mwezi julai mwaka jana ambako licha ya kuiba bastola hiyo waliiba na vitu vingine.

Kwa mujibu wa Swai,majambazi hao wakiwa na silaha za moto waliiba pia seti moja ya TV aina ya Sony yenye ukubwa wa inchi 40 ikiwa na thamani ya shilingi milioni 1.2,pete ya ndoa ya mke wake na pesa taslimu zaidi ya paundi 20,000 za Uingereza.

Hata hivyo mfanyabiashara huyo amsema kuwa wakati tukio hilo linatokea yeye hakuwepo nyumbani kutokana na kuwa uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro(KIA) ambako alikuwa akipokea wageni wake kutoka nchini Marekani.

“Kama ningekuwa nyumbani siku hiyo basi lolote ningeweza kutokea nap engine leo nisingekuwa hai maana kwa jinsi walivyoingia nyumbani ni  hakika walikuwa wamejipanga kwa lolote”.amesema.

Wakati bastola yake ikipatikana baada ya kuhusika katika tukio la mauaji huko Korogwe mkoani Tanga,seti yake ya TV ilipatikana kwa mmoja wa watuhumiwa hao wa mauaji ,Fredrick Menadi eneo la Chekereni ya Bonite mjini Moshi.

WAFIKISHWA MAHAKAMANI KWA MAUAJI YA MLINZI

Wakati huo huo,watuhumiwa hao wamefikishwa katika mahakama ya hakimu mfawidhi wa wilaya ya Korogwe mkoani Tanga wakikabiliwa na shitaka moja la mauaji ya mlinzi wa shamba hilo la Mkonge la Kwa Mduru.

Waliofikishwa mahakamani mbele ya hakimu mfawidhi Kassim Kwawa ni,Ebeni Venance Mwaipopo(27)fundi na mkazi wa Ngarenairobi mkoani Arusha na Fredrick Menadi (46) boda boda mkazi wa Chekereni ya Bonite mjini Moshi.

Wengine ni Diana Godliving binti wa miaka 24 na mkazi wa Kigogo Jijini Dar es salaam pamoja na Dismas Venance Mwaipopo pia mkazi wa Dar es salaam anayetajwa kuwa ni baba mzazi wa mshitakiwa wa kwanza.

Washitakiwa hao  walisomewa shitaka moja la mauaji na mwendesha mashitaka mkaguzi wa polisi,Richard Rweyemamu ambako wanadaiwa kutenda kosa hilo Novemba 23 mwaka jana saa 3.20 usiku.

Hata hivyo washitakiwa hao baada ya kusomewa shitaka hilo hawakutakiwa kujibu chochote kutokana na mahakama hiyo ya wilaya kutokuwa na uwezo wa kusikiliza mashauri ya mauaji na kurejeshwa  rumande katika gereza la wilaya la Korogwe lililopo Korogwe mjini.

  

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni