Jumatano, 2 Mei 2018

GOD'SLOVE MAPHIE: MDAU WA MAENDELEO ALIYEVUTIWA NA MPANGO WA MAGUFULI KUIFUFUA ATCL


TANGU aingie madarakani,Rais wa awamu ya Tano,Dk.John Pombe Magufuli amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa serikali yake inafanya mapinduzi makubwa katika kuelekea uchumi wa kati.

Rais  Magufuli amekuwa muumini wa Tanzania ya Viwanda akiamini kuwa ili Taifa lipige hatua kimaendeleo kufikia uchumi wa kati sharti sekta ya viwanda iimarishwe.

Katika kufanikisha Tanzania ya viwanda,hivi karibinu serikali ilitangaza  zabuni ya ujenzi wa mradi mkubwa wa bwawa la kuzalisha umeme katika  maporomoko ya maji yam to Rufiji yanayofahamika kama Stiegler’s  Gorge yanyopatikana ndani ya pori tengefu la Selous . 

Kwa mujibu wa Waziri wa madini,Dk.Medadi  Kalemani,mradi huo  utazalisha umeme wa kiasi cha megawati 2,100 na na utagharimu kiasi cha Dola za Marekani Bilioni 2 ambazo zitatolewa na Serikali ya Tanzania.

Dkt. Kalemani amesema malengo ya Serikali ni kuzalisha umeme kiasi cha megawati 5,000 ifikapo mwaka 2020 na megawati 10,000 ifikapo mwaka 2025 kama Sera ya Nishati ya mwaka 2015 inavyoelekeza.

"Tunataka kujenga Tanzania ya Viwanda. Tunataka ifikapo mwaka 2019-20 tufike megawati 5,000. Tanzania ya Viwanda inahitaji umeme, mradi kama huu na pia ya Kinyerezi I Extension, MW 185 Kinyerezi II MW 240 na miradi mingine itawezesha kufikia lengo letu," alisema Dkt. Kalemani.

Mbali na mkakati wa Rais Magufuli kuifanya Tanzania kuwa ya viwanda,pia amekuwa katika harakati za kuhakikisha shirika la Ndege Tanzania(ATCL)linafufuliwa kwa kiwango cha juu pamoja na ununuzi wa ndege mpya.

Lengo la serikali ya Rais Magufuli ni kuhakikisha shirika hilo la umma linarejea katika hali yake ili kuinua usafiri wa anga na kuwawezesha watanzania kuendelea kunufaika na raslimali za Taifa lao.

Hadi sasa Rais Magufuli amefanikisha ununuzi wa ndege nne zikiwamo mbili aina ya Dash8-Q400 zenye uwezo wa kubeba abiria 76 kila moja na Dash8-Q300 moja yenye uwezo wa kubeba  abiria 50.

Tayari safari za ndege za shirika hilo ambazo kwa muda mrefu zilisitishwa,zimeanza ikiwamo safari za Dar es salaam- Mbeya,Dar es salaam-Dodoma na kwingineko kwa lengo la kuwapatia huduma bora na kwa bei nafuu watanzania.
 Mdau wa maendeleo Jijini Arusha,God'slove Maphie


God’slove Maphie ni mmoja wa wadau wa maendeleo katika Jiji la Arusha ambaye ameguswa na harakati za Rais Dk.John Pombe magufuli za kulifufua shirika hilo la ndege ikiwamo ununuzi wa ndege mpya.

Katika mahojiano maalumu na mwandishi wa makala haya jijini Arusha,Maphie anasema hatua ya Rais Magufuli kulifufua shirika hilo ni ya kupongezwa na watanzania wote wapenda maendeleo.

“Mimi sitafuti ajira kwa mheshimiwa Rais,lakini ni ukweli uliowazi kuwa kitendo cha kulifufua shirika letu la ndege ni kitendo cha kupongezwa sana hasa katika kuelekea uchumi wa kati”,anasema.

Maphie anasema ilikuwa ni aibu kubwa kwa nchi kubwa kama Tanzania kutokuwa na shirika lake la ndege linalojiendesha kwa ufanisi  huku nchi ndogo kama Rwanda yenye watu wachache ikilinganishwa na Tanzania zikiwa na shirika la ndege.

Mbali na hilo pia amepongeza hatua ya serikali ya Tanzania kuzindua ujenzi wa mradi wa  rada nne ambazo zitakuwa mahususi katika kuhakikisha anga la Tanzania linakuwa salama .

“Unapokuwa huna rada za kuongoza ndege maana yake ni kwamba anga lako linakuwa haliko salama lakini kwa hatua hii ya serikali kuanza ujenzi wa rada nne ni hatua nzuri sana kwetu sisi kama taifa”,anasema.

Pamoja na kupongeza jitihada hizo za serikali ya Dk.John Pombe Magufuli kulifufua shirika la ndege na ujenzi wa rada,akashauri usimamizi mzuri wa raslimali hizo za taifa.

Anasema kama hapatakuwa na usimamizi nzuri katika uendeshaji wa ATCL,basi watanzania watarajie kurejea kule ambako shirika limetoka baada ya kukosa usimamizi mzuri .

Maphie anasema ni wajibu wa bodi ya wakurugenzi ya ATCL kuhakikisha shirika hilo halifi kwa kulisimamia vizuri ili juhudi za Rais Magufuli za kulifufua shirika hilo zilete  matunda mazuri.

“Hata wewe mwandishi wa habari ili ufanye kazi yako kwa ufanisi ni sharti uzingatie miiko ya taaluma yako na hicho ndicho watanzania wanataka kuona shirika linaendeshwa na watu wanaofuata misingi na maadili ya taaluma zao”,anasema.

Anasema kuwa,anaamini Rais magufuli akiuungwa mkono katika jitihada zake za kuwaletea maendeleo watanzania miaka michache ijayo Tanzania itapiga hatua kubwa kiuchumi na kuondokana na hali ya kuwa tegemezi.
 Moja ya Ndege za Shirika la Ndege Tanzania(ATCL) ikiwa angani.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni