Jumamosi, 26 Mei 2018

TENGENI MUDA WA KUZUNGUMZA NA MUNGU,WAKRISTO WAASWA




WITO  umetolewa kwa wakristo nchini kujenga tabia ya kutenga muda wao kuzungumza na mungu badala ya kutegemea siku  za ibaada makanisani.

Wito huo umetolewa hivi karibuni  na Makamu Mkuu wa Askofu wa Kanisa la Tanzania Assemblies of  God (TAG)Dkt .Magnus Mhiche  wakati wa Ibada ya uzinduzi wa Hema la kuabudia la Kanisa la International Christian Centre (ICC) lililoko Soweto mjini Moshi .

Dkt.Mhiche alisema,wakristo wanao wajibu wa kuzungumza na mungu pahala popote iwe makazini,safarini na hata majumbani mwao badala ya kusubiri kwenda makanisani kuhudhulia ibaada.

Askofu  Mhiche alisema kuwa kuna Wakristo wanaoheshimu majengo ya Makanisa kuliko kumuogopa Mungu mwenyewe na kwamba wanapotoka Makanisani humuacha Mungu na kuendelea na mambo yao maovu.

“Kuna watu wanapokuwa Makanisani wanaonekana ni watu waliookoka, wenye unyenyekevu, lakini ukifuatilia matendo yao na mienendo yao haiendani na ukristo wao, nawasihi sana hebu badilikeni acheni kumdhihaki Mungu, Mungu anahitaji ushirika na wewe Mkristo,”alisema  Mhiche.

Aidha Askofu  Mhiche alizungumzia umuhimu wa kutenga muda wa maombi na sala na kutoa rai kwa waamini kuacha kumdhihaki Mungu pale tu wanapokuwa kwenye nyumba za Ibada pekee, ambapo alisema kuwa wakishatoka huko huendelea kutenda dhambi.
 Makamu Mkuu wa Kanisa la TAG,Askofu Magnus Mhiche akiomba kabla ya uzinduzi wa Hema la kuabudia la Kanisa la International Christian Centre(ICC)lililopo Soweto Mjini Moshi,kulia kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro,Anna Mghwira.

“Mungu alipotuumba alitaka tuwe na ushirika na yeye, Ibada ni mfumo wa ushirika, tunapokutana kwenye makanisa yetu huo ni ushirika wako wewe na mimi,” alisema.

Alisema licha ya kuwa watu wote hujua umuhimu wa maombi, wengi wao wanaugumu wa kutenga muda kwa ajili ya maombi wakati wakiwa makazini,safarini na majumbani mwao.

Askofu Mhiche aliwakumbusha wakristo  kuwa ukweli wa moyo wa binadamu daima huwa katika maombi na kuwataka wabadilike kwa  kutenga muda wa kutafakari juu ya mema anayowatedea mwenyezi mungu.

Akawageukia maaskofu na kuwataka waendelee kuwasaidia washirika kutambua majira na nyakati za ulimwengu wa sasa katika  kipindi hiki ambacho watanzania wengi wanaendelea kulalamika ya kuwa hali ya uchumi ni ngumu.

“Mimi wakati wa utawala wa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere nilikuwa nasoma kidato cha nne,nimeshuhudia pia utawala wa Marais Mwinyi, Mkapa na Kikwete, wote hawa sikuwahi kumuona hata mmoja wao akiwagawia Watanzania fedha”, alisema.

Alisema wanaoendelea kulialia kuwa hali ni mbaya ama vyuma vimekaza hao ni wale ambao walikuwa wamezoea kuwanyonya baadhi ya watanzania ambao ni watu wa hali ya chini.

Kwa upande wake Askofu Mkuu wa Jimbo la Kilimanjaro Magharibi la Kanisa hilo, Dkt Benjamin Bukuku, alisema kuwa makanisa ya TAG yanakabiliwa na upungufu wa wachungaji hivyo kuomba wachungaji kupelekwa ili kwenda kutoa huduma ya kiroho.

“Bado Kanisa linawajibu mkubwa wa kuendelea kupata makazi ya Kanisa ya kuabudia, kujengwa kwa hema hili kutawezesha waumini kuweza kupata huduma ya kiroho mahali hapa,” alisema.

Naye  mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira amelipongeza kanisa la International Christian Centre (ICC), lililoko chini ya TAG, kwa kuona umuhimu wa kujenga hema hilo.

Mkuu huyo wa mkoa alisema kuwa madhehebu ya dini yamekuwa msaada mkubwa kwa serikali katika kuwahudumia watanzania na kuachana na mambo maovu.

Aidha mkuu huyo wa mkoa alisema kuwa serikali inathamini mchango wa taasisi za dini katika kudumisha amani, utulivu na mshikamano hapa nchini.

Mghwira alisema ya kuwa serikali inatambua huduma za kijamii zinazotolewa na taasisi za dini ikiwemo Elimu, Afya, miradi ya maji na miradi mingine ya kimaendeleo.

Alisema serikali itaendelea kutoa michango ya hali na mali pale inapowezekana ili kuhakikisha raia wake wanapata maendeleo na wanaishi kwa furaha na utulivu.


Awali akitoa taarifa ya ujenzi wa hema hilo Mchungaji kiongozi wa Kanisa la International Christian Centre (ICC) Askofu Mstaafu wa TAG Glorius Shoo alisema  hema hilo limegharimu kiasi cha shilingi milioni 100 hadi kukamilika kwa ujenzi huo.

Pia  mchungaji Shoo alimpongeza Rais Dkt John Magufuli kwa kuwapatia eneo hilo ili waweze kujenga jengo ambalo litatumika kutolea huduma za kiroho na za kimwili mahali hapo.
 
 Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Anna Mghwira akisalimiana na Viongozi wa Kanisa la TAG muda mfupi kabla ya kukata utepe kuashiria uzinduzi wa Hema la kuabudia la kanisa International Christian Centre(ICC) eneo la Soweto mjini Moshi ambalo lipo chini ya TAG.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni