Alhamisi, 4 Januari 2018

MTOTO WA NDESAMBURO AWAPOZA WALIMU,WAFUNGWA MIAKA MITATU



Na Charles Ndagulla,Moshi

MAHAKAMA ya hakimu mkazi mjini Moshi,imewahukumu kutumikia kifungo cha miaka mitatu jela walimu wawili wa shule ya Msingi ya Mwereni iliyopo wilaya ya Hai baada ya kukutwa na hatia ya kuhamisha umiliki wa shamba la shule isivyo halali.



Hukumu hiyo imetolewa januari 3 mwaka huu na kaimu hakimu mfawidhi  wa mahakama hiyo,Aidan Mwilapwa  baada ya kuwatia hatiani washitakiwa hao .



Walimu waliotiwa hatiani na kuhukumiwa kifungo hicho ni Mwalimu mkuu wa shule hiyo,Onesmo Ernest Kinyaiya na mwalimu mkuu msaidizi wa shule hiyo,Apolinary Denke Pantaleo.

Shamba hilo lilitolewa na walimu hao  kwa mtoto wa Marehemu Philemon Ndesamburo aitwaye Tomm ambaye ni mmoja wa wakurugenzi wa kampuni ya Rahisi General Marchant Ltd ambayo ni kampuni tanzu ya makampuni ya Rahisi Group ya mjini Moshi.



Walimu hao walifikishwa mahakamani hapo na kusomewa mashitaka na waendesha mashitaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(Takukuru),Barry Galinoma akisaidiana na Furahini Kibanga.



Kwa mujibu wa hati ya mashitaka iliyosomwa makahamani hapo na waendesha mashitaka hao wa Takukuru,wlimu hao walishitakiwa kwa kosa la kuhamisha umiliki wa shamba la shule hiyo kwenda kwa kampuni ya Rahisi General Marchant Ltd bila idhini ya kamishna wa Ardhi.



Kulingana na hati hiyo ya mashitaka,walimu hao hawakuwa na mamlaka hayo kwa mujibu wa kifungu cha 17(5) cha sheria ya ardhi ya vijijini sura ya 14 kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2002.



Hivyo  uhamishaji huo ulikuwa kinyume na kifungu cha 31 cha sheria ya Kuzuia na Kupambana na rushwa namba 11 ya mwaka 2007 hivyo mahakama hiyo kuwatia hatiani katika shauri hilo la jinai namba 3 la mwaka 2016.



Katika hukumu hiyo,walimu hao walihukumiwa kifungo cha miaka mitatu jela au faini ya shilingi laki tano na baada ya mahakama kuwatia hatiani walimu hao walinusurika kwenda jela baada ya ndugu walikuwa wamefurika mahakanai hapo kuchangishana fedha na kuwalipia faini.



Baada ya hukumu hiyo,Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa(Takukuru) mkoani Kilimanjaro,imetoa taarifa kupitia kwa Mkuu wa Taasisi hiyo mkoani hapa,Holle Makungu kuwa itafuatilia kwa mwajiri wa walimu hao ili kuhakikisha wanaondolewa kwenye utumishi wa umma.





KARANI MAHAKAMA YA MWANZO  MBARONI KWA RUSHWA YA LAKI MOJA.



Katika tukio jingine,mtego ulioandaliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(Takukuru),umefanikiwa kumnasa karani mmoja wa mahakama ya Mwanzo iliyopo Maili Sita wilaya ya Hai .



Karani huyo,Rose Jonathan Urassa(58),alinaswa na Takukuru baada ya kudai rushwa ya shilingi laki moja ili amsaidie mshitakiwa katika shauri la jinai namba 69/2017 kupitia kwa hakimu anayesikiliza shauri hilo.



Taarifa ya Takukuru mkoani Kilimanjaro iliyotolewa kwa vyombo vya habari leo Januari 4 na kusainiwa na Mkuu wa Takukuru mkoa(RBC),Holle Makungu imeeleza kuwa,karani huyo aliomba fedha hizo ili hakimu anayesikiliza shauri hilo aweze kutoa hukumu ya upendeleo kwa mshitakiwa.



“Baada ya taarifa hizo kupokelewa,mtego wa rushwa uliandaliwa na aliweza kukamatwa januari 3 mwaka huu akiwa amepokea fedha hizo katika eneo hilo  la mahakama ya mwanzo,Hai,Rose atafikishwa mahakamani mara uchunguzi utakapokamilika”,imesema taarifa hiyo.



Takukuru imetoa  onyo kwa baadhi ya makarani na wahudumu wa mahakama wanaoendekeza tabia ya kuomba na kupokea rushwa kwa kisingizio cha kutumwa na waheshimiwa mahakimu wabadili tabia hiyo.



Kamanda Makungu katika taarifa yake hiyo kwa vyombo vya habari,ametoa rai kwa makarani na wahudumu wa mahakama katika mkoa wa Kilimanjaro wanaoendelea  na tabia hiyo mwisho wao wa  kufanyakazi katika utumishi wa umma kwa mwaka huu 2018 utakuwa mwisho wao.



Pia alitoa wito kwa wananchi wanaodaiwa rushwa na baadhi ya makarani na wahudumu wa mahakama kwa kisingizio cha  kutumwa na waheshimiwa mahakimu,watoe taarifa kwa taasisi hiyo ili iweze kuboresha mahakama kwa kuwaondoa wachache wanochafua sura za mahakama.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni