Jumatatu, 3 Novemba 2014

MUWSA: TATIZO LA MAJI MOSHI MJINI MWISHO DESEMBA



MAMLAKA  ya maji safi na Usafi wa Mazingira Moshi Mjini(MUWSA) inakamilisha utekelezaji wa miradi mitatu ya maji ambayo itaondoa kero ya muda mrefu ya upatikanaji wa maji safi kwa wananchi ifikapo desemba mwaka huu.
 MKURUGENZI WA MUWSA, CYPRIAN LUHEMEJA

 

Hayo yamo kwenye taarifa ya hali ya huduma ya maji safi iliyotolewa jana na mkurugenzi wa mamlaka hiyo,Cyprian Luhemeja katika mkutano maalum na waandishi wa habari uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa mamlaka hiyo.

Miradi hiyo inahusisha visima viwili vya CCP na Kili Tank pamoja na chanzo cha maji kilichopo mto karanga ambacho maji yake yatazinufaisha kata za Pasua,Boma mbuzi,matindigana na mabogini na maeneo ya katikati ya mji ambapo wananchi wapatao 20,000 watanufaika na mradi huo.

MABOMBA YA MAJI KATIKA HIFADHI SALAMA YA MUWSA
Alisema mradi huo wa maji kutoka chemchem ya chanzo cha maji mto karanga unategemewa kuongeza mita za ujazo 2,592 kwa siku katika mfumo wa kusambazia maji pindi mradi utakapokamilika. 

Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo,uzalishaji wa maji katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita ni wastani wa mita za ujazo, 34,944 kwa siku ikilinganishwa na mahitaji ya mita za ujazo 45,082 kwa siku.

Mamlaka hiyo pia imefanya ukarabati wa kilometa 11.8 za mabomba katika mkakati wa kuhakikisha maji yanayoongezwa kwenye mfumo wa kusambazia maji hayapotei kwa kupitia kwenye maomba chakavu na hivyo kuwafikia wateja wengi zaidi.

AIR VALVE KATIKA CHANZO CHA MAJI, KARANGA MJINI MOSHI
Mkurugenzi huyo alisema katika taarifa yake kuwa,matarajio ya mamlaka yake katika kipindi cha Oktoba 2014 na Juni 2015 ni kuanza ujenzi wa chemchem ya maji ya Ndesuo iliyopo Kibosho wilaya ya Moshi vijijini katika mpango wake wa kuboresha zaidi huduma ya maji safi.

Mpango mwingine wa mamlaka hiyo ni kumalizia uchimbaji wa visima viwili vya maji vilivyopo kata ya Longuo ambavyo mamlaka hiyo ilikabidhiwa na manispaa ya Moshi ikiwamo uwekaji wa umeme,pampu,motor na mabomba.

Chini ya mpango huo,mamlaka hiyo imelenga kufanyia ukarabati mtandao wa majisafi kwa  kilometa 14.9 pamoja na kufanyia upanuzi wa mtandao kwa kilometa 40.65 katika sehemu mbalimbali za mji ambazo bado hazijafikiwa na mtandao.
 WAANDISHI WA HABARI MJINI MOSHI

KNCU: OFISI YA MRAJIS VYAMA VYA USHIRIKA KIKWAZO


Chama  Kikuu cha Ushirika mkoani Kilimanjaro(KNCU),kimeishutumu ofisi ya mrajis wa vyama vya ushirika nchini na kudai ofisi hiyo ni kikwazo katika ustawi  wa ushirika kutokana na kuyumba katika utoaji wa  maamuzi.
 DKT. AUDAX RUTABANZIBWA AKIZUNGUMZA KATIKA MKUTANO MKUU MAALUM WA KNCU, MJINI MOSHI

Shutuma hizo zilitolewa mwishoni mwa wiki na mwenyekiti wa chama hicho,Maynard Swai katika mkutano mkuu maalumu ulioitishwa na mrajis wa vyama vya ushirika nchini kujadili hoja za ukaguzi ambazo ofisi hiyo imedai chama hicho kimeshindwa kuzijibu kwa muda mrefu.

Mwenyekiti huyo alidaia kuwa,ofisi hiyo ya mrajis imekuwa ikitoa maamuzi tata ikiwamo kuzuia uuzwaji wa shamba kubwa la kahawa la Gararagua ambalo chama hicho kililenga kuliuza ili kuweza kulipa mkopo wa benki ya CRDB,madeni ya vyama vya msingi na kuimarisha hali ya kifedha ya chama hicho.

Alidai kuwa,pamoja na kuishirikisha ofisi hiyo katika mchakato mzima wa uuzwaji wa shamba hilo na ofisi hiyo ya mrajis kutoa ruhusa ya kuuzwa kwa shamba hilo kwa barua ya machi 27 mwaka huu,ofisi hiyo ilisitisha uuzwaji wa shama hilo .

Kwa mujibu wa mwenyekiti huyo,kitendo cha ofisi hiyo ya mrajis kuwa na maamuzi tata ni uvunjifu wa sheria namba 6  ya ushirika ya mwaka 2013 kifungu cha 132(3) kinachoweka bayana kuwa mtu yeyote anayekwaza au kuingilia shughuli za ushirika na kuisababishia hasara atawajibika kwa hasara hiyo.

Kutokana na mkanganyiko huo wa maamuzi ,chama hicho kimedai kuwa kitalazimika kulipa riba na marejesho  ya milioni 250 mapema mwezi ujao baada ya mwezi mei kufanya hivyo kwa kiwango kama hicho .

Akizungumzia hoja hizo,mwenyekiti huyo alidai kuwa,hoja hizo ni batili kwa mujibu wa kifungu cha 55(9) cha sheria namba 6 ya ushirika ya mwaka 2013 kinachoweka wazi kuwa,hesabu zikishawasilishwa na kujadiliwa na kisha kupitishwa na mkutano mkuu,uamuzi wao dhidi ya hesabu hizo ni wa mwisho na kwamba hoja hizo ni batili kutokana na kuwasilishwa nje ya muda kama sheria inavyotamka.

Kuhusu mgogoro wa shamba la Lyamungo,chama hicho kimedai kuwa,ofisi hiyo ya mrajis imeshindwa kutekeleza maagizo ya aliyekuwa waziri wa ushirika,George Kahama kwamba shamba hilo ni mali ya KNCU  katika barua yake ya Oktoba 21 mwaka 2005.

Chama hicho kimedai kuwa,pamoja na kuendelea kumkumbusha mrajis juu ya uamuzi huo wa waziri,hakuna hata barua moja iliyojibiwa huku shamba hilo likiendelea kukaa bila kuwanufaisha wanachama.
 WAJUMBE WA MKUTANO MKUU WA KNCU 2014

Jumatatu, 30 Juni 2014

CHARLES NDAGULLA, MWANAHABARI MKONGWE TANZANIA



Charles Ndagulla ni Mwandishi habari Mkongwe nchini Tanzania, ambaye ameshiriki katika mafunzo mbalimbali yakiwemo ya habari za uchunguzi . 
 Alizaliwa Machi 1, 1970 kijiji cha Ng’wankuba, wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza.