Jumatatu, 3 Novemba 2014

VIJANA WAHANGA WAKUBWA TATIZO LA AJIRA NCHINI



Suala  la  ajira hapa nchini limeelezwa kuwa ndiyo tatizo kubwa  katika jamii  huku wahanga wakubwa  wakiwa ni vijana  kutokana na kundi hilo kuongoza kwa aslimia 61.7 ya watanzania wote.

MWANZILISHI/MTENDAJI MKUU WA TAASISI YA TANZANIA SME GROWTH CENTER, VICTOR TESHA

Kauli hiyo ilitolewa mwishoni mwa wiki na Mwanzilishi na mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Tanzania SME Growth Center,Victor Tesha wakati akitoa elimu ya ujasiriamali kwa makundi ya kina mama na vijana katika kata za Uru Kishumundu na Uru Kaskazini.

Alisema kuwa kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012  kundi la vijana ndilo linaloongoza  kwa wingi  kuliko makundi mengine ya Wazee na Watoto ambako inaonyesha vijana kati ya umri wa miaka 15 – 35 wanafikia asilimia 61.7 .

 Mtendaji huyo mkuu wa Taasisi hiyo alikuwa alitoa elimu hiyo ikiwa ni mpango wa taasisi yake kuwawezesha kina mama na vijana waliojiunga katika vikundi vya ujasiriamali kunufaika na mikopo itakayotolewa na taasisi yake katika wilaya za Moshi Vijijini na Mjini pamoja na mkoa wa Arusha.

Akitoa elimu hiyo,Tesha alisema ufumbuzi wa tatizo la ajira litapungua  na kufanikiwa pale jamii itakapobaini  kiini cha tatizo hilo na kiini hicho kimesambaa kwa kiasi kipi suala ambalo linahitaji wadua binafsi na serikali kuangalia namna ya kulitatua.
  
Katika kukabiliana na tatizo hilo  la ajira kwa vijana,mtendaji huyo alisema kuwa,vijana wanatakiwa kuwa na mlengo wa mabadiliko kwa kuamini kuwa ajira si lazima uajiliwe tu bali hata kwa kujiajiri kwa kufanya biashara ndogondogo na kuachana na kasumba ya kuchagua kazi.

 Alisema kwa mujibu wa ripoti ya shirika la kazi dunia( ILO) ya mwaka 2011 inaonyesha kuwa  asilimia 78.8 ya vijana kote duniani  hawakuwa na ajira, viwango vya vijana waliokosa ajira ilifikia asilimia 12.6% mwaka 2013 na inategemewa kupanda hadi kufikia 12.8% ifikapo mwaka  2018.

Aliongeza kuwa ripoti hiyo imemzindua  na kuwa na wazo la kutatua tatizo la ajira kwa kutafuta taasisi ambazo zinaweza kutoa mikopo ya masharti nafuu kabisa ya  kuwawezesha vijana kujikwamua kimaisha kwa kujiajiri wenyewe.

Alisema watakaonufaika na mikopo hiyo yenye riba nafuu ni vijana na kina mama waliojiunga katika vikundi vya kuanzia watu kumi ambao watajiandikisha na vikundi vyao kutambulika kisheria.

Chini ya mpango huo kabla ya kunufaika na mikopo hiyo,vijana na kina mama  watapewa mafunzo ya kuwajengea uwezo kibiashara ili kupambana na matatizo yanayoweza kujitokeza, kujua njia za kifasaha za kuendesha biashara .

Kwa mujibu wa Tesha,mikopo hiyo itatolewa  kwa mfumo wa vifaa badala ya pesa ambako kila kikundi kitaainisha mahitaji yake  kulingana na biashara watakayofanya kwa pamoja ambako mikopo hiyo inatarajia kuanza kutolewa mwezi ujao.

MUWSA: TATIZO LA MAJI MOSHI MJINI MWISHO DESEMBA



MAMLAKA  ya maji safi na Usafi wa Mazingira Moshi Mjini(MUWSA) inakamilisha utekelezaji wa miradi mitatu ya maji ambayo itaondoa kero ya muda mrefu ya upatikanaji wa maji safi kwa wananchi ifikapo desemba mwaka huu.
 MKURUGENZI WA MUWSA, CYPRIAN LUHEMEJA

 

Hayo yamo kwenye taarifa ya hali ya huduma ya maji safi iliyotolewa jana na mkurugenzi wa mamlaka hiyo,Cyprian Luhemeja katika mkutano maalum na waandishi wa habari uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa mamlaka hiyo.

Miradi hiyo inahusisha visima viwili vya CCP na Kili Tank pamoja na chanzo cha maji kilichopo mto karanga ambacho maji yake yatazinufaisha kata za Pasua,Boma mbuzi,matindigana na mabogini na maeneo ya katikati ya mji ambapo wananchi wapatao 20,000 watanufaika na mradi huo.

MABOMBA YA MAJI KATIKA HIFADHI SALAMA YA MUWSA
Alisema mradi huo wa maji kutoka chemchem ya chanzo cha maji mto karanga unategemewa kuongeza mita za ujazo 2,592 kwa siku katika mfumo wa kusambazia maji pindi mradi utakapokamilika. 

Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo,uzalishaji wa maji katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita ni wastani wa mita za ujazo, 34,944 kwa siku ikilinganishwa na mahitaji ya mita za ujazo 45,082 kwa siku.

Mamlaka hiyo pia imefanya ukarabati wa kilometa 11.8 za mabomba katika mkakati wa kuhakikisha maji yanayoongezwa kwenye mfumo wa kusambazia maji hayapotei kwa kupitia kwenye maomba chakavu na hivyo kuwafikia wateja wengi zaidi.

AIR VALVE KATIKA CHANZO CHA MAJI, KARANGA MJINI MOSHI
Mkurugenzi huyo alisema katika taarifa yake kuwa,matarajio ya mamlaka yake katika kipindi cha Oktoba 2014 na Juni 2015 ni kuanza ujenzi wa chemchem ya maji ya Ndesuo iliyopo Kibosho wilaya ya Moshi vijijini katika mpango wake wa kuboresha zaidi huduma ya maji safi.

Mpango mwingine wa mamlaka hiyo ni kumalizia uchimbaji wa visima viwili vya maji vilivyopo kata ya Longuo ambavyo mamlaka hiyo ilikabidhiwa na manispaa ya Moshi ikiwamo uwekaji wa umeme,pampu,motor na mabomba.

Chini ya mpango huo,mamlaka hiyo imelenga kufanyia ukarabati mtandao wa majisafi kwa  kilometa 14.9 pamoja na kufanyia upanuzi wa mtandao kwa kilometa 40.65 katika sehemu mbalimbali za mji ambazo bado hazijafikiwa na mtandao.
 WAANDISHI WA HABARI MJINI MOSHI

KNCU: OFISI YA MRAJIS VYAMA VYA USHIRIKA KIKWAZO


Chama  Kikuu cha Ushirika mkoani Kilimanjaro(KNCU),kimeishutumu ofisi ya mrajis wa vyama vya ushirika nchini na kudai ofisi hiyo ni kikwazo katika ustawi  wa ushirika kutokana na kuyumba katika utoaji wa  maamuzi.
 DKT. AUDAX RUTABANZIBWA AKIZUNGUMZA KATIKA MKUTANO MKUU MAALUM WA KNCU, MJINI MOSHI

Shutuma hizo zilitolewa mwishoni mwa wiki na mwenyekiti wa chama hicho,Maynard Swai katika mkutano mkuu maalumu ulioitishwa na mrajis wa vyama vya ushirika nchini kujadili hoja za ukaguzi ambazo ofisi hiyo imedai chama hicho kimeshindwa kuzijibu kwa muda mrefu.

Mwenyekiti huyo alidaia kuwa,ofisi hiyo ya mrajis imekuwa ikitoa maamuzi tata ikiwamo kuzuia uuzwaji wa shamba kubwa la kahawa la Gararagua ambalo chama hicho kililenga kuliuza ili kuweza kulipa mkopo wa benki ya CRDB,madeni ya vyama vya msingi na kuimarisha hali ya kifedha ya chama hicho.

Alidai kuwa,pamoja na kuishirikisha ofisi hiyo katika mchakato mzima wa uuzwaji wa shamba hilo na ofisi hiyo ya mrajis kutoa ruhusa ya kuuzwa kwa shamba hilo kwa barua ya machi 27 mwaka huu,ofisi hiyo ilisitisha uuzwaji wa shama hilo .

Kwa mujibu wa mwenyekiti huyo,kitendo cha ofisi hiyo ya mrajis kuwa na maamuzi tata ni uvunjifu wa sheria namba 6  ya ushirika ya mwaka 2013 kifungu cha 132(3) kinachoweka bayana kuwa mtu yeyote anayekwaza au kuingilia shughuli za ushirika na kuisababishia hasara atawajibika kwa hasara hiyo.

Kutokana na mkanganyiko huo wa maamuzi ,chama hicho kimedai kuwa kitalazimika kulipa riba na marejesho  ya milioni 250 mapema mwezi ujao baada ya mwezi mei kufanya hivyo kwa kiwango kama hicho .

Akizungumzia hoja hizo,mwenyekiti huyo alidai kuwa,hoja hizo ni batili kwa mujibu wa kifungu cha 55(9) cha sheria namba 6 ya ushirika ya mwaka 2013 kinachoweka wazi kuwa,hesabu zikishawasilishwa na kujadiliwa na kisha kupitishwa na mkutano mkuu,uamuzi wao dhidi ya hesabu hizo ni wa mwisho na kwamba hoja hizo ni batili kutokana na kuwasilishwa nje ya muda kama sheria inavyotamka.

Kuhusu mgogoro wa shamba la Lyamungo,chama hicho kimedai kuwa,ofisi hiyo ya mrajis imeshindwa kutekeleza maagizo ya aliyekuwa waziri wa ushirika,George Kahama kwamba shamba hilo ni mali ya KNCU  katika barua yake ya Oktoba 21 mwaka 2005.

Chama hicho kimedai kuwa,pamoja na kuendelea kumkumbusha mrajis juu ya uamuzi huo wa waziri,hakuna hata barua moja iliyojibiwa huku shamba hilo likiendelea kukaa bila kuwanufaisha wanachama.
 WAJUMBE WA MKUTANO MKUU WA KNCU 2014