Jumamosi, 10 Machi 2018

BREAKING NEWS: BAA YA MEKU'S MOSHI YAFUNGWA,WATAKIWA KUFUNGASHA NDANI YA SAA 24

 Na Charles Ndagulla,Moshi

HALMASHAURI ya Manispaa ya Moshi imeifunga Baa maarufu ya MEKU'S ya mjini Moshi kutokana na kukiuka sheria ya udhibiti wa mazingira pamoja na sheria ya afya ya jamii.


Baa hiyo imefungwa kwa mujibu wa barua ya Manispaa  hiyo ya machi 8 mwaka huu kwenda MEKU'S iliyosainiwa na Danford Kimenya kwa niaba ya Mkurugenzi wa Manispaa hiyo.

"Yah:amri halali inayokutaka kufunga biashara ya baa na Restaurent inayotolewa chini ya sheria ya udhibiti wa mazingira Na.20 ya mwaka 2004 na sheria ya afya ya jamii Na.1 ya mwaka 2009",inasomeka barua hiyo ambayo tumeichapisha hapa chini.

 
 "Unatahadharishwa kuwa kukaidi kutekeleza matakwa ya amri hii kutailazimisha ofisi kuchukua hatua kali za kisheria dhidi yako bila kukupa onyo lolote ikiwa ni pamoja na kukufikisha mahakamani",inaonya barua hiyo.

Pamoja na Baa hiyo kujengwa ndani ya kituo cha mafuta ambayo ni hatari kwa usalama wa watumiaji wa baa hiyo,bado mamlaka husika ziliziba masikio na kufumbia uvunjaji huo wa sheria.

Uchunguzi wetu ulidhibitisha pasipo na shaka yoyote kuwa,MEKU'S haikufuata taratibu za mipango miji ikiwamo kujengwa bila kuwa na michoro iliyoidhinishwa na idara ya mipango miji ya manispaa ya Moshi.

Hata ofisi ya Mkuu wa kikosi cha zimamto imewahi kukiri kutokuwa na michoro ya Baa hiyo hatua ambayo ilidhibitisha uchunguzi wetu. 

Baa hiyo pamoja na mgahawa vilijengwa ndani ya mita kumi kutoka zilipo pampu za mafuta kwenye kituo hicho cha mafuta jambo ambalo ni hatari kwa usalama wa watu na mali zao endapo kungetokea mlipuko wa moto.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni