Jumatano, 17 Desemba 2014

JAJI WEREMA AJIUZULU KWA KASHFA YA ESKROW, IKULU YABARIKI

 
M
wanasheria Mkuu wa Serikali ya Tanzania, Jaji Frederick Werema amejiuzulu nafasi yake hiyo kuanzia jana, Jumanne, kufuatia sakata la uchotaji wa fedha kutoka akaunti ya ESCROW ambapo zaidi ya dola milioni 120 zilihamishwa.

Mwanasheria mkuu, pamoja na baadhi ya wanasiasa na maafisa waandamizi wa serikali walituhumiwa kuhusika kwa namna moja au nyingine kufanikisha kufanyika kwa miamala haramu ya fedha za Akaunti ya Escrow ya Tegeta.

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Dar es Salaam, imesema Rais Jakaya Kikwete alikubali ombi hilo la kujiuzulu kwa Mwanasheria Mkuu huyo wa Serikali.

Katika barua yake kwa Rais Kikwete, Jaji Werema alisema ameomba kujiuzulu kwa sababu ushauri wake kuhusiana na suala ya Akaunti ya Tegeta Escrow haukueleweka na umechafua hali ya hewa. 

Rais Kikwete amemshukuru Jaji Werema kwa utumishi wake ulioongozwa na uaminifu na uadilifu.

Itakumbukwa kwamba sakata la Akaunti ya Escrow liliibuliwa bungeni na mmoja wa wabunge wa bunge la Tanzania, David Kafulila na kusababisha mjadala mkali na kuamua Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kupewa jukumu la kuchunguza kashfa hiyo.

Baada ya uchunguzi kuwasilishwa katika mkutano wa bunge uliomalizika mwishoni mwa mwezi Novemba, kamati hiyo ilikuja na maazimio manane kuhusu taarifa ya ukaguzi maalum kuhusiana na miamala iliyofanyika katika akaunti ya Escrow ya Tegeta pamoja na umiliki wa kampuni ya IPTL.

Miongoni mwa maazimio ya bunge yaliwataja baadhi ya wanasiasa, mwanasheria mkuu, maafisa waandamizi wa serikali, majaji, wakuu wa taasisi za umma, viongozi wa dini, mawakili wa kujitegemea na watu binafsi kuhusika katika kashfa hii na hivyo kuagiza mamlaka zinazohusika kuwachukulia hatua za kisheria wahusika na wengine kuondolewa katika nyadhifa zao za kuteuliwa.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni