Jumamosi, 18 Novemba 2017

DAKTARI MAWENZI HOSPITAL APANDA KIZMBANI KWA RUSHWA YA LAKI UNUSU




TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU),   imewafikisha mahakamani Daktari wa Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Kilimanjaro, Mawenzi Dkt. Deogratias Godfrey Urio pamoja na Muuguzi wa Hospitali hiyo, Naomi Shayo kwa kosa la kuomba na kupokea Rushwa ya shilingi 150,000. 

Washitakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo jana Ijumaa mbele ya hakimu mkazi ,Pamela Meena  na kusomewa mashitaka na wakili na mwendesha mashitaka wa Takukuru mkoa wa Kilimanjaro,Barry Galinoma  akisaidiwa na Caroline Lugenge.

Katika shauri hilo la jinai namba  2/2017 ,washitakiwa hao wanashitakiwa chini ya kifungu cha  15 kifungu kidogo cha kwanza A na kifungu kidogo cha pili  cha sheria namba 11 ya kupambana na rushwa ya mwaka 2007.

Kwa mujibu wa hati ya mashitaka iliyosomwa na mawakili hao wa Takukuru,washitakiwi hao wanadaiwa kuwa kati ya Novemba 10 na 15 mwaka huu kwa pamoja wakiwa watumishi wa Serikali katika hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Kilimanjaro Mawenzi walidai rushwa kiasi cha shilingi 150,000.

Wanadaiwa kuomba kiasi hicho cha fedha kutoka kwa  Stanley Samson ili waweze kumfanyia upasuaji wa uvimbe katika kizazi ndugu yake aitwaye Lightness Samson, huku wakitambua kuwa ni kinyume na sheria.
  
Galinoma alidai kuwa, kosa la pili linamhusu mshitakiwa wa kwanza ambaye ni Dkt. Deogratias Godfrey Urio ambapo alitenda kosa hili kinyume na kifungu cha  15 kifungu kidogo cha kwanza A na kifungu kidogo cha pili cha   sheria ya kuzuia na kupambana na Rushwa namba 11 ya mwaka 2007.

Ilidaiwa mahakama hapo kuwa mshitakiwa wa kwanza  Daktari Urio  akiwa katika baa ya Mombasa  High way iliyopo Mji Mdogo wa Himo akiwa kama mwajiriwa wa Katibu Tawala mkoa wa Kilimanjaro, na kama Daktari wa Hospitali ya Mawenzi alipokea kiasi cha shilingi 150,000/- kama rushwa kutoka kwa Stanley Samson kwa ajili ya kumfanyia upasuaji wa uvimbe katika kizazi ndugu yake aitwaye Lightness Samson.

Baada ya kusomewa mashitaka yao,washitakiwa wote  walikana mashitaka yao, ambapo upande wa Jamuhuri ulieleza kuwa upelelezi wa kesi hiyo unaendelea na kuomba kupangiwa tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa kwa kesi hiyo. 

Washitakwia  waliachiliwa kwa dhamana baada ya kutimiza masharti ya dhamana yaliyowataka kila mmoja  kuwa na wadhamini wawili wanaoaminika na  watakaosaini fungu la dhamana ya shilingi milioni moja kila mmoja,kesi hiyo   imepangwa kutajwa tena Desemba 18 mwaka huu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni