Jumamosi, 11 Novemba 2017

USIMAMIZI DHAIFU WA RASLIMALI ZA MAJI WAYAKOSESHA MABILIONI YA FEDHA MABONDE YA MAJI.



Na Charles Ndagulla,Moshi

OFISI ya Mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali(CAG),imeibua madudu yanayosababisha mabonde ya maji kukosa mabilioni ya fedha yatokanayo na mapato kutoka kwa watumiaji wa maji nchini.

Miongoni mwa madudu hayo ni kutokuwepo na udhibiti kwa watumiaji wa maji hatua ambayo imesababisha baadhi ya watumiaji wa maji kuzidisha viwango vya uchukuaji wa maji tofauti na  ilivyoainishwa kwenye vibali vyao.

Hayo yamo kwenye mada iliyowasilishwa na mkaguzi ufanisi kutoka ofisi ya CAG,Rebecca Mahenge kwenye warsha ya siku moja iliyolenga kujadili ripoti ya CAG toleo la Mwananchi kwa mwaka wa fedha uliomalizika machi 31 mwaka huu 2017.

Warsha hiyo ilifanyika mjini Moshi hivi karibuni na  kushirikisha asasi zisizo za kiserikali kutoka mikoa ya Manyara,Arusha,Kilimanjaro na Tanga pamoja na wanahabari wa mkoa wa Kilimanjaro.

Madhumuni ya ukaguzi wa ufanisi kwa mujibu wa mkaguzi huyo ni kutoa tathimini ya kiwango  ambacho thamani ya fedha yaani uwekevu,tija na ufanisi huzingatiwa na taasisi za serikali zinapotumia raslimali katika kutekeleza majukumu yake.

Alisema kuwa,mamlaka ya maji safi na uondoshaji maji taja Jijini Mwanza(MWAUWASA)ilizodisha maji kwa aslimia 70 baada ya kutumia lita za ujazo 90,000 kwa siku badala ya lita za ujazo 50,000 kwa siku.

Amesema kitendo hicho kiliikosesha mapato Bodi ya Bonde la maji ziwa Victoria ya shilingi Milioni 41 kama malipo ya ziada kutoka kwa watumiaji waliozidisha viwango vya maji.

Ripoti hiyo ambayo imo kwenye kitabu kidogo imebainisha kuwa,Bonde la mto Wami/Ruvu limepoteza mapato yanayokadiliwa kufikia shilingi Milioni 814 kutokana na visima vilivyochimbwa  bila kufuata utaratibu rasmi katika wilaya ya Ilala mkoa wa Dar es salaam  na hivyo kutotambuliwa na Bodi ya maji ya Bonde la mto Ruvu.

Mkaguzi huyo wa ufanisi amesema kuwa  kwa mujibu wa ukaguzi  uliofanywa na ofisi ya CAG,umebaini kuwa kati ya visima 2,888 vilivyopo wilaya ya Ilala,ni visima 262 pekee ndio vipo kwenye orodha ya usajili.

Amesema mabonde manne yalikosa shilingi Bilioni mbili sawa na aslimia 40 ya kiasi cha shilingi bilioni tano walizotakiwa kukusanya katika kipindi cha miaka mitano cha 2011-2012 hadi 2015/2016.

Ukaguzi huo ambao ulihusu usimamizi na udhibiti wa uchukuaji wa maji kutoka vyanzo vya maji, ulihusisha mabonde manne ambayo  ni  bonde la mto Pangani,Bonde la ziwa Victoria,bonde la Mto Wami/Ruvu na bonde la kati.

Amesema kuwa,udhaifu katika ukusanyaji wa mapato umesababisha wenye vibali vya kuchukua maji katika mabonde hayo kutokufuata sheria na makubaliano waliyoingia kati yao na mamlaka za mabonde.

“Kumekuwepo na udhaifu katika ukusanyaji wa mapato yatokanayo na ada wanazolipa wenye vibali vya kuchukua maji katika mabonde,hali hii imechangia bodi za mabonde kukosa fedha za kutekeleza majukumu yake.”,amesema.

Aidha imebainika katika ukaguzi huo kuwa,sera ya maji ya mwaka 2009 na sheria namba 11 ya mwaka 2009 inayohusu usimamizi wa Raslimali za maji ambayo inaelekeza uzingatiaji wa uwepo wa maji na akiba ya maji kwa ajili ya mazingira,haizingatiwi katika utoaji wa vibali vya maji.
 
 Ripoti hiyo ikapendekeza wizara ya maji na umwagiliaji kuyaagiza mabonde ya maji kuzingatia matumizi  endelevu katika vyanzo  vya maji ikiwamo kuhakikisha kunakuwepo mpango wa pamoja wa usimamizi wa raslimali za maji unaotumika katika mabonde yote.

Pia ikapendekezwa kuimarishwa kwa  udhibiti katika ukusanyaji wa mapato pamoja na wachukuaji wa maji wasio na vibali na wale wanaozidisha viwango vilivyoainishwa katika vibali vyao.

Lengo la ukaguzi huo  wa CAG ni kubaini ukubwa wa tatizo la uhaba wa maji unaotokana na uharibifu wa vyanzo vya maji hivyo kusababisha migogoro kwa watumiaji wa maji.

Katika ukaguzi huo pia mapungufu kadhaa yalijitokeza ikiwamo kutokuwepo na mipango jumuifu wa usimamizi wa raslimali za maji katika mabonde hayo kwa kuwashirikisha wadau wote.

Hali hiyo imetajwa kusababisha utoaji wa vibali pasipo kuzingatia kiasi cha maji kinachopatikana katika mabonde husika kutokana na kutokuwepo kwa udhibiti kwa watumiaji wa maji.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni