Jumatatu, 13 Novemba 2017

MASKINI LULU,ATUPWA JELA MIAKA MIWILI KIFO CHA KANUMBA



 DAR ES SALAAM

Baada ya Mahakama kumkuta Msanii Elizabeth Michael ‘Lulu’ na hatia ya kuua bila kukusudia na kuhukumiwa kifungo cha miaka miwili jela, Wakili wa Msanii huyo, Peter Kibatala amesema wanakusudia kukata rufaa ili kumsaidia mteja wake. 

Hukumu hiyo imetolewa mapema leo katika Mahakama Kuu Kanda ya  Dar es Salaam  ambapo Lulu amekutwa na hatia ya kumuua bila kukusudia Msanii mwenzake marehemu Steven Kanumba mwaka  2012 maeneo ya Sinza, Dar es Salaam. 
 
Muda mfupi baada ya kutolewa kwa hukumu hiyo,  Wakili Kibatala amesema wamepokea hukumu hiyo lakini utaratibu wa kukata rufaa unafanyika ili kumnusuru mteja wake, ambapo ushahidi wa mazingira ndio umemtia hatiani mshtakiwa kwasababu yeye alikuwa mtu wa mwisho kuwa na marehemu wakati tukio hilo linatokea. 

“Kwa kifupi ni kwamba tutakata rufaa, wakati rufaa inaandaliwa tutaomba dhamana mchakato wake ni wa kisheria”, amesema Wakili Kibatala.

Elizabeth Michael kwa mara ya kwanza alipelekwa Mahakama ya Kisutu iliyopo Dar es salaam, akishtakiwa kuua bila kukusudia tarehe 7 mwaka 2012, wakati huo akiwa chini ya umri wa miaka 18, ambapo leo amesomewa hukumu ya kufungwa jela miaka 2.

Kabla ya kusoma hukumu hiyo, Jaji Sam Rumanyika aliIeleza kuwa Mahakama  imetoa hukumu hiyo kwa kuzingatia ushahidi wa mazingira kwasababu hakukuwepo na ushahidi wa moja kwa moja wa kuhusika na mauaji ya marehemu Kanumba.

 "Ushahidi wa mazingira ni ushahidi ambao mstakiwa alikubali kwamba yeye ni  mtu wa mwisho kuwa na marehemu ambapo mshtakiwa alikuwa na Uhusiano wa kimapenzi na marehemu kwa miezi minne" 

“Ushahidi wa mazingira unaweza kutumika kama msingi pekee wa kumtia hatiani mshtakiwa tena mshtakiwa pekee, Sasa ninapokwenda kuangalia maelezo ya mshtakiwa kama yanakidhi vigezo nilivyosema awali". Ameeleza Jaji Rumanyika.

Aidha Jaji Rumanyika amesema  ameridhishwa na ushaidi wa mashaidi wanne wa upande wa mashtaka na amemtia hatiani Elizabeth maarufu kama ‘Lulu’ chini ya kifungu cha Sheria cha 195 cha sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai.
 
Ushahidi wa Mazingira ni nini?
 
Mtaalamu wa Sheria, Gilbert Daudi kutoka mkoa wa Kigoma anasema ushahidi wa mazingira ni ushahidi wa nyongeza ambao unatumika  sambamba na ushahidi wa moja kwa moja. Anaeleza kuwa, 

“Ushahidi wa kimazingira ni kwamba  tukio limetokea sehemu fulani, mtu amekuwepo sehemu hiyo ya tukio anahusishwa mazingira kwa sababu yeye yuko hapo kwa muda huo. Huo ushahidi wa mazingira lazima uwepo ushahidi wa nyongeza kuweza kumtia mtu hatiani”, 

Anasema ushahidi wa mazingira huchukuliwa kama ni ushahidi wa nyongeza ambao unatumika kama mtu alikutwa eneo la tukio lakini haimaanishi kuwa mtu huyo amefanya hilo tukio na mahakama ikijiridhisha mtuhumiwa hutiwa hatiani na kuhukumiwa. 

Akitoa maoni yake juu ya hukumu iliyotolewa leo kwa Msanii Lulu amesema Mahakama imetenda haki kulingana na ushahidi walioupata lakini Mawakili wa mtuhumiwa  wana nafasi ya kukata rufaa kama hawajaridhishwa na hukumu hiyo.

Anaamini kuwa Mawakili wa Lulu wakikata rufaa wana uwezekano wa kushinda na Msanii huyo akaachiwa huru kutokana na aina ya ushahidi uliotumika ambao kwa tafsiri ya kisheria ni ushahidi wa nyongeza na sio wa moja kwa moja.

Chanzo:fikrapevu.com



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni