Bei
ya mafuta ya petroli, dizeli na ya taa nchini inazidi kushuka kutokana na
kuporomoka kwa bei ya mafuta ghafi katika soko la dunia tangu Juni mwaka jana.
Mkurugenzi
Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (Ewura), Felix Ngamlagosi
alisema jana kuwa bei ya rejareja ya petroli kuanzia leo imeshuka kwa Sh74,
dizeli kwa Sh62 na mafuta ya taa kwa Sh54.
Bei
hizo zinashuka wakati kukiwa na mjadala mkali kuwa bei zilizopo sasa hazisadifu
hali halisi ya kuporomoka kwa mafuta ghafi yanayouzwa kwa Dola 50 za Marekani
kwa pipa.
Ngamlagosi
alisema bei hizo mpya zimekokotolewa kutokana na bei ya mafuta ghafi na kwamba
huenda ikapungua zaidi siku zijazo.
Alisema
kwa sasa bei ya jumla za nishati hiyo zimepungua ukilinganisha na mwezi
uliopita, kwani kwa lita petroli imepungua kwa Sh73.75, dizeli Sh62.08 na
mafuta ya taa kwa Sh54.34.
“Be
za mafuta safi ya petroli kwa tani katika soko la dunia imepungua kwa Dola 249
za Marekani, dizeli kwa Dola 189 na mafuta ya taa kwa Dola 180.
Kufuatia
bei hizo mpya, petroli katika vituo vya Dar es Salaam haitazidi Sh1, 955,
dizeli Sh1,846 na mafuta ya taa Sh1,833.
Kutokana
na gharama kubwa za usafirishaji, wakazi wa Kyerwa Kagera ndiyo watakaokuwa
wakinunua petroli kwa bei ya juu zaidi kwa Sh2,192, dizeli Sh2, 083 na mafuta
ya taa Sh2,070.
Ngamlagosi
alisema ni vigumu bei iliyopo ikaendana na bei ya sasa katika soko la dunia kwa
kuwa mafuta yanayoingia nchini hununuliwa kwa bei ya mwezi mmoja uliopita na
kwamba kushuka kwa thamani ya Shilingi kumechangia pia.
“Watu
wanatakiwa wafahamu kuwa gharama za kodi hazibadiliki. Pia kuna malipo ya
usafirishaji na usambazaji, vyote vinachangia karibu asilimia 40 ya gharama za
mafuta.
“Asilimia
60 tu ndiyo inayoathirika na kushuka au kupanda kwa bei ya mafuta ghafi katika
soko la dunia,” alisema.
Mhadhiri
wa Shule ya Biashara ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDBS), Dk Goodluck Urassa
alisema bei hizo mpya zinaendana na hali halisi ya soko la dunia.
CHANZO: MWANANCHI
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni