Siku
chache baada ya matokeo ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa kuonyesha kuwa CCM,
imeporomoka, Mbunge wa Bumbuli, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Wizara ya
Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba amewataka wanachama wa
chama hicho kujiandaa kisaikolojia kwa matokeo yoyote yanayoweza kutokea katika
Uchaguzi Mkuu Oktoba mwaka huu.
“Wana-CCM
wanatakiwa kujiandaa kisaikolojia kwani walizoea ushindi wa asilimia 90 au 80
(wa kishindo), huu ulikuwa ushindi wa nyuma. Tusishangae tukipata ushindi wa
asilimia 50, 60, 57 au 70 ni kitu cha kawaida kutokana na kukua kwa demokrasia
hususan ushindani wa vyama vingi vya siasa kuanza kuimarika.
Kauli
hiyo ya Makamba imekuja wakati matokeo ya serikali za mitaa yakionyesha kuwa
CCM imeporomoka kutoka ushindi wa asilimia 91.7 mwaka 2009 hadi 79.8 katika
uchaguzi wa mwaka jana na upinzani ukipanda kutoka asilimia nane mwaka 2009
hadi takriban 20 mwaka jana.
Akizungumza
jana katika mahojiano na kipindi cha ‘Power Breakfast’ cha Redio ya Clouds na
baadaye kufafanua baadhi ya hoja alipozungumza na mwandishi wetu, Makamba
alisema matokeo ya uchaguzi huo ni ishara kwamba kwa umri wa miaka 22 sasa,
mfumo wa vyama vingi vya siasa umeanza kuimarika.
“Hata
ushindi wa asilimia 81 tulioupata katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa bado ni
mkubwa na hata kama tungepata asilimia 70 haupunguzi uhalali wa uongozi. Kusema
CCM itang’oka madarakani, hapana, bado wananchi wanakiamini tena sana,” alisema
Makamba.
Makamba ambaye pia ni Naibu Waziri wa Sayansi na
Teknolojia, alizungumzia pia namna ya kuwapata wagombea wa urais na kusema
mwaka huu ndiyo utapima ukomavu wa chama katika harakati za kumpata mrithi wa
Rais Jakaya Kikwete.
Makamba ambaye Julai 2, mwaka jana akiwa London,
Uingereza alitangaza nia ya kuwania urais kupitia CCM, alisema mwaka 1995
mgombea alipatikana kwa malezi ya Mwalimu Julius Nyerere, mwaka 2000 aliendelea
aliyekuwapo. Alisema mwaka 2005 ilikuwa kama 1995 lakini mwaka huu ni tofauti
na vipindi vingine kabisa.
CHANZO:
MWANANCHI
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni