Jumatatu, 26 Januari 2015

MWENYEKITI CCM MAREKANI AFUNGWA MIEZI 18 NA KULIPA FAINI YA SH. MILIONI 92.4



Mwenyekiti wa CCM wa tawi la Texas, Houston nchini Marekani, Simon Makangula amehukumiwa kifungo cha mwaka mmoja na nusu jela na kulipa faini ya zaidi ya Sh92.4 milioni kwa kosa la kughushi nyaraka za ulipaji wa kodi.

Makangula ambaye ni mmiliki wa kampuni ya kutoa huduma za malipo ya kodi iitwayo Mshale Investment & Tax Service, alihukumiwa Ijumaa katika Mahakama ya Wilaya na Jaji Gray Miller kwa udanganyifu huo wa kuwasaidia wateja wake kughushi nyaraka za kodi ya mapato, kwa mujibu wa tovuti ya click2houston.com.

Wakili wa serikali nchini humo, Kenneth Magidson pamoja na Lucy Cruz, wakala maalumu wa kitengo cha uchunguzi wa makosa ya kihalifu katika masuala ya mapato ya Marekani, kwa nyakati tofauti waliiambia mahakama kuwa Makangula alimsaidia mmoja wa wateja wake ambaye ni raia wa Marekani kutayarisha malipo ya kodi yasiyo halali.

Sambamba na kifungo cha mwaka mmoja na nusu, pia Makangula anatakiwa kulipa faini ya Dola 51,645 sawa na Sh92.4 milioni.

Oktoba 15, mwaka jana, Makangula alikiri kosa hilo mbele ya hakimu Miller na kuwa malipo ya kodi hiyo yalikuwa na udanganyifu katika vipengele kadhaa, yakiwamo katika makadirio na idadi ya wategemezi wa mlipakodi, mambo yaliyosababisha hasara ya Dola 9,731 za Marekani (Sh17.3 milioni).

Pia, katika kesi hiyo, Makangula alikiri kuwa alimsaidia mteja wake kughushi kuwa yeye ndiye mmiliki pekee wa biashara hiyo, hatua iliyosaidia watu wengine, washirika wa mteja wake, wakwepe kulipa kodi.

Kampuni ya Makangula inajishughulisha na huduma za ulipaji wa kodi, uhasibu, mfumo wa ulipaji wa kodi za mapato, biashara za ardhi, kodi za majengo na ushauri wa masuala ya kodi ya mapato.

CHANZO: MWANANCHI

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni